Saturday, June 9, 2012

UKOSEFU WA USINGIZI NI HATARI KWA AFYA YAKO



KITENDO cha kukosa usingizi mara kwa mara wakati wa kulala kuna weza kuonekana ni jambo ambalo halina madhara kiafya, lakini ukweli ni kwamba unapokosa usingizi, hasa kwa muda mrefu, kuna athari kubwa katika afya yako yote, hata kama unakula na kufanya mazoezi vizuri.
Madhara ya ukosefu usingizi huathiri mfumo mzima wa mwili, mathalan, mbali ya kuathiri kinga ya mwili na kuongeza hatari ya kupatwa na magonjwa ya saratani, ukosefu wa usingizi huweza kusababisha madhara mengine yafutayo:
HATARI YA KUPATWA NA UGONJWA WA MOYO
Unapokosa usingizi, mfumo wa uzalishaji homoni huvurugika ambapo uzalishaji wa homoni za ‘stresi’ (stress hormones) huongezeka. Pia husababisha vidonda vya tumbo na hali ya kusikia njaa hata kama umetoka kula muda mfupi. Uko hatarini kusumbumbuliwa na hasira na ghadhabu kila mara.
ONGEZEKO LA SHINIKIZO LA DAMU
Ukosefu wa usingizi huchangia pia ongezeko la shinikizo la damu, pia huchangia kuzeeka kwa mtu kutokana na kuvurugika kwa uzalishaji wa homoni za ongezeko la umri. Humfanya mtu kuonekana mzee ili hali bado ana umri mdogo.
KUZIDISHA TATIZO LA UKOSEFU WA CHOO
Ukosefu wa usingizi huchangia pia tatizo la ukosefu wa choo na huweza hata kusababisha kifo kama tatizo likiwa sugu.
EPUKA KUTUMIA DAWA ZA USINGIZI
Kama unasumbuliwa na tatizo la ukosefu wa usingizi, jua kwamba hauko peke yako. Utafiti uliofanywa hivi karibuni nchini Marekani na Taasisi ya Taifa ya Usingizi (National Sleep Foundation –NSF), umegundua kuwa kati ya watu 10, ni wanne tu hupata usingizi mzuri kila wiki.
Pamoja na kuonekana kwa athari nyingi za kukosekana kwa usingizi, lakini utakuwa unajiweka katika madhara na hatari zaidi iwapo utalazimisha kupata usingizi kwa kumeza dawa za usingizi, kwa sababu ni hatari na mara nyingi dawa hizo huwa hazisaidii kuondoa tatizo.
JINSI YA KUFANYA ILI UPATE USINGIZI
Kwa asili yake, kichocheo cha usingizi mwilini kijulikanacho kama ‘melatonin’ hupatikana kwa ulaji wa mboga za majani na matunda mbalimbali ya kuongeza virutubisho mwilini na hupatikana pia kwa kupata mwanga wa jua wa kutosha wakati wa mchana. Hivyo huna haja ya kumeza vidonge badala yake zingatia uzalishaji wa kirutubisho hicho kwa mlo na mwanga wa jua.
Ili kujiwekea mazingira mazuri ya kupata usingizi mzuri, unashauriwa kuepuka kufanya yafuatayo muda mfupi kabla ya kupanda kitandani kulala:
Epuka kuangalia TV au kompyuta muda mfupi au saa moja kabla ya kulala, kwani teknolojia hizi siyo nzuri sana kwa macho kutokana na mwanga wake, hasa kwa mtu mwenye matatizo ya kupata usingizi.
Epuka kulala huku taa inawaka, hakikisha unalala huku taa zote zikiwa zimezimwa, licha ya mwanga wa taa usiku kusababisha madhara mengine, lakini huchangia kuharibu mtiririko wa usingizi. Hata uamkapo usiku kwenda msalani, ikiwezekana usiwashe taa ili kuepuka kuvuruga usingizi wako.
Usilale karibu na vifaa vya umeme na vyenye sumaku kama vile saa, simu, au redio kwani huchangia kudhoofisha uzalishaji wa homoni za usingizi. Hata saa yako yenye ‘alarm’ ya kukuamsha, unashauriwa kuiweka mbali nawe kabisa.
Mwisho, hakikisha unakuwa na ratiba ya kulala inayoeleweka na hakikisha unalala muda huohuo kila siku. Kwa kawaida mtu anatakiwa kulala kati ya saa tatu na saa nne usiku. Iwapo utazingatia vyote vilivyoelezwa hapo juu, bila shaka utaweza sasa kulala usingizi mnono.

No comments:

Post a Comment

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...