Tuesday, June 19, 2012

GARI LA RAY LAUNGUA MOTO USIKU



Vincent Kigosi ‘Ray’.
GARI la msanii maarufu wa filamu hapa nchini, Vincent Kigosi ‘Ray’, juzikati liliwaka moto usiku na kuteketea katika Viwanja vya Leaders vilivyopo Kinondoni jijini Dar.

Kikiongea na Ijumaa Wikienda, chanzo chetu makini ambacho kilikuwa jirani na eneo la tukio wakati gari hilo linaungua, kilisema kuwa wakiwa wanasikiliza muziki uliokuwa ukipigwa katika gari hilo kwa mbali, walishtuka kuliona linafuka moshi eneo la mbele, majira ya saa tano usiku.

“Kiukweli tulishtuka sana kuona gari la Ray likiwaka moto bila kujua nini chanzo… mpaka tunafika sehemu gari hilo lilipokuwa limeegeshwa, tulikuta tayari kila kitu kimeungua,” kilisema chanzo hicho ambacho ni msanii wa filamu.

Ray alipotafutwa kwa njia ya simu, alikiri kutokea kwa ajali hiyo na kueleza kuwa baadaye gari hilo lilikokotwa na kupelekwa katika Kituo cha Polisi Oysterbay na baada ya uchunguzi kukamilika, lilipelekwa gereji tayari kwa matengenezo.

“Kweli ajali ilitokea pale Leaders Club na kusababisha kila kitu kilichokuwa ndani ya gari kuteketea. Lilipelekwa Oysterbay Polisi kwa ajili ya uchunguzi na ulipokamilika lilipelekwa gereji ya Wachina ya Sinza kwa matengenezo zaidi ingawa kwa hali liliyonalo sijui kama litatengenezeka.

“Nasubiri majibu kutoka TRA, kama wataweza kuligharamia matengenezo itakuwa sawa lakini ikishindikana basi itabidi nilipwe gari jipya kwani lilikuwa na bima kama ilivyo sheria ya TRA kwenye ajali kama hizi,” alisema Ray.

No comments:

Post a Comment

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...