Saturday, April 28, 2012

TASWIRA YA KANUMBA NYUMBANI: Mama KANUMBA apata mshtuko...





Katika tukio bichi kabisa, mapema wiki hii, mama Kanumba alipata mshtuko uliomsababishia kupandwa na presha baada ya kuingia chumbani kwa marehemu na kukumbana na taswira ya picha ya marehemu.

Kwa mujibu wa chanzo chetu, mama huyo alishatoa agizo kwa wanafamilia kuzifunika ukutani picha zote za marehemu zilizomo ndani ili asiweze kumwona mwanaye ambaye aliaga dunia ghafla.


Ikasemekana kuwa siku ya tukio la wiki hii, mama Kanumba alifungua mlango wa chumba cha marehemu na kukutana uso kwa uso na picha kubwa iliyokuwa ukutani jambo ambalo lilimshtua sana.

“Alikuwa anaingia chumbani kwa marehemu, ile anafungua tu mlango ukutani akakumbana na picha ya marehemu, akashtuka, presha ikampanda. Maskini, sijui nani aliyeigeuza ile picha wakati mwenyewe alishaamuru picha zote zifunikwe ili asizione,” kilisema chanzo chetu.

Kikaendelea: Tangu alipopata taarifa za kifo cha mwanaye, mama Kanumba amekuwa mtu wa kupandwa na presha, kupoteza fahamu na kutundikiwa dripu, hivyo anatakiwa kuombewa sana.

MLOLONGO WA MATUKIO
Kwa mujibu wa taarifa za ndani, tukio la kwanza la mama huyo kupoteza fahamu ni lili lillilotokea Uwanja wa Ndege wa Mwalimu Julius Nyerere, Dar es Salaam, Aprili 8, mwaka huu alipotua akitokea Bukoba, Kagera ambako ndiko alikopatia taarifa za kifo cha mwanaye. (angalia picha ya ukurasa wa kwanza).


Waombolezaji waliokwenda kumpokea, akiwemo mama wa nyota wa filamu, Vincent Kigosi ‘Ray’, Mary Kigosi walifanya kazi ya ziada kumpatia huduma ya dharura ili arejee katika hali yake ya kawaida.

MAISHA NYUMBANI KWA KANUMBA
Kuna ushahidi wa kutosha kwamba ndani ya nyumba ya marehemu ambapo mama Kanumba yupo kwa sasa, Sinza ya Vatican City Hotel, jijini Dar picha zote za marehemu, hata ile iliyotumika kwenye utambulisho wa jeneza na meza ya viongozi kuandika kitabu cha kumbukumbu, zimefunikwa ukutani.


Ndugu mmoja wa karibu alisema mbele ya mama wa marehemu kuwa mama huyo amekuwa akipata tatizo la presha kupanda mara kwa mara na kutundikiwa dripu ambapo katika moja ya vyumba ndani ya nyumba hiyo kuna chupa za dripu zilizokwishatumika.

ANAISHI KWA USHAURI
Habari zaidi zikasema kuwa, mama huyo ameshauriwa kuishi na maji ya kunywa karibu ili kupambana na tatizo la presha za mara kwa mara.

Watu wa karibu wanasema mara kadhaa mama wa marehemu anakuwa kawaida, lakini linapokuja suala la kumzungumzia mwanaye, hubadilika sura na kuagiza maji au soda ili kujiweka sawa.

“Mara nyingi hataki mambo yanayomhusu marehemu, ikitokea anawahi kusema ongeeni na Seth (akimaanisha mdogo wa marehemu) ili asijiingize kwenye mawazo ya kumuwaza mwanaye.

KINACHOMTESA KWA SASA
Kwa mujibu wa ndugu wa karibu, mama huyo kwa sasa anateswa na uhaba wa watu, inapotokea hakuna watu wanaoingia zaidi ya yeye na familia yenye watu wasiozidi sita, ndipo anapokubali kuwa mwanaye amefariki dunia na kuzikwa,  hivyo hurejesha kilio upya.

STAILI YA KIFO NDIYO INAYOMTESA ZAIDI MAMA 
Jumatano ya wiki hii, paparazi wetu alipata nafasi ya kuongea na mwanafamilia mmoja wa marehemu, nje ya nyumba, ambapo alimuuliza maoni ya mama wa marehemu kuhusiana na kifo cha mwanaye ambapo alisema:

“Mama wa marehemu anakiri kifo kipo, lakini kwa mwanaye anaona afadhali angeugua hata kwa siku moja akili ingekubali kuwa kuna kupona na kufa, lakini ile kuzimika kama mshumaa kunamsumbua zaidi.

WITO KWA VIONGOZI WA DINI 
Kifo kimeumbwa, lakini kusahau pia kumeletwa kwa wanadamu, hivyo baadhi ya watu wamewataka viongozi wa dini kwenda nyumbani kwa marehemu na kumfanyia maombi mama Kanumba ili Mungu afute kumbukumbu za kifo cha mwanaye haraka.

No comments:

Post a Comment

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...