Thursday, August 4, 2011

BABU LOLIONDO APINDULIWA NA MTOTO...





Mtoto Subira Ally (12), Mkazi wa Kijiji cha Malema, Kata ya Maratani, wilayani Nanyumbu, mkoani Mtwara ameonekana kumpindua Babu wa Loliondo, Mchungaji Ambilikile Masapile (pichani) kwa kupata wateja wengi ambao wanakwenda kutibiwa.

Kupinduliwa kwa Babu kumetafsiriwa na watu baada ya kuonekana sasa nyumbani kwake Kijiji cha Samunge hakipati wageni wengi kama ilivyo Kijiji cha Malema anakokaa Subira ambako  wageni kutoka mikoa mbalimbali na nchi jirani hufurika kila kukicha.

Akizungumza na mwandishi wa habari hii hivi karibuni, mtoto Subira alisema kuwa siku moja ,  Aprili mwaka huu akiwa amelala alioteshwa ndoto iliyokuwa ikimuelekeza kuwa anatakiwa atoe tiba kwa njia ya kikombe kwa kutumia mzizi wa mti uitwao Mkong’oto unaopatikana hapo nyumbani kwao, hivyo kumjulisha mama yake mkubwa anayeishi naye.

“Niliambiwa kuwa dawa hiyo itakuwa inatibu Ukimwi, kisukari, kuponya vipofu, viziwi, na wote ambao miili yao itakuwa imekufa ganzi au kupooza,” alisema Subira.

Aliongeza kuwa dawa hiyo ya kikombe alioteshwa kuwa iwe ikinunuliwa kwa gharama ya shilingi 500. Alipoulizwa ni watu wangapi ambao amewatibu tangu alipoanza kazi hiyo alisema ni wengi sana.

“Wagonjwa ni wengi sana ambao wamepata kikombe na wanaendelea kufika hapa nyumbani,” alisema huku akiwa na mama yake mkubwa aliyefahamika kwa jina moja la Binti Ismail.






WAGENI TOKA NJE YA NCHI

Subira alisema licha ya kutibu wananchi wa Tanzania, amekuwa akipokea wageni wengine kutoka nje ya nchi kama vile Msumbiji na Malawi.

Aliongeza kuwa licha ya wagonjwa wengi kutoka Tanzania bara, amepokea wengine kutoka  Visiwani Zanzibar na anakumbuka mmoja alikuwa na matatizo ya miguu ambayo ilikuwa imekufa  ganzi kwa miaka mitano. “Sasa mgonjwa huyo wa Zanzibar ganzi imekwisha na anatembea vizuri, amemshukuru sana Mungu.” Mama mkubwa wa binti huyo, aliyefahamika kwa jina la Binti Ismaili alithibitisha mwanaye kuoteshwa na kutoa tiba hiyo.

MASHUHUDA

Naye mama mmoja  aliyejitambulisha kwa jina moja tu la Sharifa  mkazi wa Tandika Mikoroshini  jijini Dar es Salaam aliyezungumza na mwandishi wetu hivi karibuni alisema kuwa, alikuwa muathirika wa ugonjwa wa Ukimwi lakini baada ya kutumia dawa ya mtoto huyo na kwenda kupima ameonekana hana virusi vya maradhi hayo.

“Baada ya kutumia dawa ya Mkong’oto nimepona,nilikwenda kupima katika Hospitali ya Maratani mkoani Mtwara  na kuthibitishiwa na daktari aliyenipima aitwae Dk.Namihambi  kuwa sina virusi. Nangoja kupima mara ya pili kwa uhakika zaidi,” alisema.

Aidha, baba mmoja ambaye aliomba jina lake kuhifadhiwa alisema kuwa alikuwa na ugonjwa wa Ukimwi lakini sasa hana baada ya kupimwa katika Hospitali ya Mkomaindo, Masasi.

WAZIRI WA AFYA ALICHOSEMA

Mara baada ya Babu Masapile kutangaza kuoteshwa kutoa tiba ya magonjwa sugu, watu wengi wameibuka kutoa tiba hiyo na wananchi kufurika kupata kikombe.

Hata hivyo, wiki iliyopita gazeti hili lilimkariri Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, Dk. Hadji Mponda akisema kuwa katika tafiti za kitaalamu dawa za mitishamba hazijathibitishwa kutibu Ukimwi.

Kauli hiyo ilitolewa na waziri huyo wakati anazindua Kituo cha Matibabu ya Wagonjwa wa Ukimwi na Mafunzo katika Hospitali ya Mnazi Mmoja, jijini Dar es Salaam hivi karibuni.

Dk. Mponda alisema wagonjwa wa Ukimwi wanatakiwa kutumia dawa za kurefusha maisha (ARV) na akawataka waende kwenye vituo vya afya kupewa.“Wagonjwa wanaokwenda kupata tiba asili waache kwa kuwa bado zinafanyiwa utafiti,” alisisitiza Waziri Mponda.

No comments:

Post a Comment

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...