Saturday, October 22, 2011

WEMA DIAMOND SASA BASI; WEMA AVUA PETE RASMI....




Aliyekuwa mchumba wa mwanamuziki wa Bongo Fleva, Naseeb Abdul ‘Diamond’, mlimbwende Wema Isaac Sepetu ameivua rasmi pete ya uchumba kufuatia kupigwa chini na msanii huyo...

Ishu hiyo ya kusikitisha, ilijiri Jumatano ya Oktoba 19 mwaka huu, saa chache baada ya kujiridhisha na taarifa za kuachwa kwake.

Wema aliivua pete hiyo ya dhahabu na kuibwaga sakafuni akiwa ndani ya chumba nambari 35, Hoteli ya Lamada iliyopo Ilala, jijini Dar es Salaam ambako amepiga kambi na wenzake kwa ajili ya kurekodi filamu.

Aidha, baada ya tukio hilo, msanii nyota wa muvi za Kibongo, Elizabeth Michael ‘Lulu’ aliiokota na kuivaa kwenye kidole husika huku akisema ‘anaosha nyota’.

“Hee, ngoja niivae miye nioshee nyota, jamani! Mh,” alisikika akisema Lulu licha ya kwamba wakati huo, Wema alikuwa akibubujikwa machozi.

Mpaka mapaparazi wetu wanaondoka eneo la tukio, Wema alikuwa bado akilia huku akisema anajuta kuvishwa pete na Diamond ambaye amemuacha njia panda.

Alisema katika maisha yake hajawahi kuachwa, Diamond amemfanyia tukio la ajabu sana na haamini masikio yake achilia mbali macho.

Jumapili ya Oktoba 2 mwaka huu, ndani ya Maisha Club, jijini Dar es Salaam, Diamond alimvisha Wema pete ya uchumba tukio ambalo lilishuhudiwa na mashabiki wao kibao.

Oktoba 18 mwaka huu, ndani ya Hoteli ya Lion, Sinza jijini Dar es Salaam, Diamond aliwaambia waandishi wa habari kwamba, ameamua kummwaga Wema kufuatia jaribio lake la kutaka kumtenganisha na mama yake mzazi.

Kwa maana hiyo basi, Wema amedumu na pete katika kipindi cha siku 16 tu....

No comments:

Post a Comment

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...