Tuesday, October 25, 2011

SAA 18 ZA MWISHO ZA MWISHO ZA GADDAFI


KUNA mvutano kuhusu mazishi ya marehemu Kanali Muammar Gaddafi, watu wa kabila la kiongozi huyo wa zamani wa Libya, wanadai mwili wa ndugu yao ili wauzike kwa heshima, wakati Baraza la Mpito linaweka ngumu na kusisitiza kwamba atazikwa kwa siri kubwa.

Ijumaa Wikienda, limenasa maisha ya Gaddafi saa 18 kabla ya kifo chake pamoja na danadana za mwili wa kiongozi huyo ambaye neno lake, harakati zake na fedha alizomwaga katika ufadhili, ndivyo viliwezesha kuundwa kwa Umoja wa Afrika.


Jumamosi iliyopita, Mwenyekiti wa Baraza la Mpito (NTC), Mustafa Mohammed Abdul Jalil alitarajiwa kwenda jijini Misrata kutoa tamko kuhusu mazishi hayo.

Kwa mujibu wa mtu anayedaiwa alikuwa mlinzi wa Gaddafi kabla ya kumgeuka dakika za mwisho, saa 18 kabla kiongozi huyo wa zamani wa Libya kufariki dunia, alizitumia kusali na kuweka mikakati ya kuhama Jiji la Sirte.

Mlinzi huyo (jina limehifadhiwa) alisema kuwa katika saa hizo 18, Gaddafi alizungumza na wanajeshi wachache waliokuwa wamebaki wanamlinda na kuwaambia kwamba hategemei kurudi kutawala Libya na hadhani kama ana maisha marefu.
Hata hivyo, jina la mlinzi huyo limefichwa ili kukwepa hasira za watu wanaompenda Gaddafi kulipa kisasi. 

Aliongeza kusema: “Aliwaambia wapigaji kwamba wakipata nafasi warudi kuitetea Libya na wasikubali vibaraka wa Marekani na Uingereza wafilisi mali za Walibya.”

Alisema kuwa saa tatu kabla Gaddafi na timu yake, hawajaanza kutoroka, alizungumza na wanaye kwa muda mrefu lakini akawasisitiza: “Msiumie wala msifedheheke, wakati mwingine Shetani hutumia nguvu na kufunika haki dhidi ya batili.”

NENO LA MWISHO
Mlinzi huyo alisema, Gaddafi alijitetea kwa maneno mengi ili asiuawe lakini kauli maarufu aliitoa kwa njia ya kuuliza, “je, ninyi wanangu, mnaifahamu haki kwenye uongo?”

SAFARI YA KIFO
Alhamisi iliyopita (Oktoba 20, 2011), Gaddafi na timu yake, wakiwa kwenye magari ya kifahari, walikuwa wanahama kutoka Jiji la Sirte kuelekea mpakani. Inadaiwa walitaka kutorokea nje ya nchi, ingawa taarifa nyingine zinadai kiongozi huyo aligoma kuondoka na kusisitiza anangoja kufa kwenye ardhi aliyozaliwa.

Saa 2:30 asubuhi (saa za Libya), vikosi vya Nato na Ufaransa viliyashambulia kwa mabomu magari ya msafara wa Gaddafi. Magari 15 yaliharibiwa kwenye mashambulizi hayo, Gaddafi na timu yake walikwenda kujificha kwenye daraja la mtaro.

5:05 asubuhi, NTC ilitangaza kuwa ngome ya Gaddafi imekwisha na kilichobaki ni kutafuta masalia.
8:00 mchana, baada ya mapambano ya risasi kwisha, Gaddafi aligundulika yupo kwenye daraja la mtaro wa maji machafu amejificha.

8:45 mchana mwanaume mmoja mkazi wa Sirte aliliambia Shirika la Utangazaji la Reuters kuwa alimuona Gaddafi akipigwa risasi tumboni kwa bastola yenye ukumwa wa 9mm.

8:56 mchana, Reuters ilitangaza kuwa Gaddafi alifariki dunia kutokana na majeraha baada ya mapigano ya risasi.

9:00 mchana, wapiganaji wa NTC walianza kuzunguka mitaani wanashangilia kukamatwa na kuuawa kwa Gaddafi.
10:31 alasiri, AFP ilitangaza kuwa mtoto wa Gaddafi, Muttasim amekutwa ameuawa jijini Sirte.

11:52 jioni, mwili wa Gaddafi ulifikishwa Misrata.

1:50 jioni, Aljazeera ilitangaza kuwa mtoto wa Gaddafi, Saif al Islam naye ameuawa kwenye mashambulizi hayo. Ingawa taarifa za baadaye zinasema kuwa Saif mikono yake ilikatika katika mashambulizi.

No comments:

Post a Comment

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...