Thursday, January 26, 2012

WATOTO WAWILI WAUAWA, WANYOFOLEWA VIUNGO VYA MWILI JIJINI MBEYA..



Mwili wa marehemu Silvia Isaya (5) aliyeuawa kisha viungo vya mwili wake kunyofolewa ulimi, jicho la upande wa kushoto, sehemu za siri na mguu wake wa kushoto kuvunjwa ukiwa umefunikwa kwa kitenge, kutokana na kuharibika vibaya hivyo kushindwa kuoneshwa.
Wanafunzi wa Shule ya Msingi Nsenga jijini Mbeya wakitoka kushuhudia mwili wa mwanafunzi mwenzao wa darasa la kwanza, Silvia Isaya (5) alieuawa kisha viungo vya mwili wake kunyofolewa ulimi, jicho la upande wa kushoto, sehemu za siri na mguu wake wa kushoto kuvunjwa.
Mwenyekiti wa Kijiji cha Nsenga Bwana Gibson Mwaselela (mwenye koti la rangi ya Samawati ), Baadhi ya wananchi wa Nsenga jijini Mbeya wakishuhudia mwili wa mwanafunzi wa darasa la Kwanza Silvia Isaya (5) alieuawa kisha viungo vya mwili wake kunyofolewa ulimi, jicho la upande wa kushoto, sehemu za siri na mguu wake wa kushoto kuvunjwa.

WIMBI la mauaji dhidi ya watoto limezidi kutanda mkoani Mbeya baada ya watoto wawili kuuawa katika nyakati tofauti na watu wasiojulikana na kisha kunyofolewa baadhi ya viungo vya mwili huko Wilaya ya Rungwe na Mbeya.

Kufuatia tukio hilo jumla ya wananchi 14 walikamatwa na Jeshi la Polisi lakini machifu waliingilia kati, ambapo mtu mmoja aitwaye Joseph Mwangolobe (40 - 45) , mkazi wa Kiwira alijitokeza na kukiri kuwa ndiye aliyehusika na mauaji hayo chumbani kwake.

Jeshi la polisi lilifanya kazi ya ziada kumnusuru Joseph asiuawe na wananchi wenye hasira kali baada ya wananchi hao kutaka kulipiza kisasi, na familia yake imelazimika kuhama ikiwa chini ya ulinzi wa polisi.

Baba mzazi wa mtoto Silvia Isaya (5), Bwana Isaya Samson Mwalyego amesema alimwacha mwanawe Silvia majira ya saa 11:00 jioni Januari 13, mwaka huu alipokuwa anakwenda kazini Hoteli ya Silver Coin, wakati mama yake akienda kutafuta mahitaji ya nyumbani kwa ajili ya mlo wa usiku.

Mama mzazi alipomaliza kupika alimtafuta mwanae pasipo mafanikio hivyo alitoa taarifa kwa Mtendaji wa kijiji cha Nsenga, Bwana Meshack Mwaipasi ambapo walitafuta usiku huo bila mafanikio.

Asubuhi majira ya saa 2 kamili Januari 24, mwaka huu, mwili wa mtoto huyo ulipatikana katika shamba la mahindi Kitongoji cha Isenyela Kata ya Nsenga ukiwa umeondolewa baadhi ya viungo na mwili wa mtoto huyo ulichukuliwa na kupelekwa katika Hospitali ya Rufaa kwa uchunguzi zaidi.

Kamanda wa Polisi Advocate Nyombi amethibitisha kutokea kwa tukio hilo na kwamba uchunguzi unafanyika ili kuweza kuwabaini waliohusika na tukio hilo la kikatili.
 

No comments:

Post a Comment

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...