Wednesday, October 10, 2012

VENGU BADO HALI TETE...






HALI ya afya ya staa wa vichekesho nchini, Joseph Shamba ‘Vengu’ ni tete na habari zilizolifikia zinasema afya yake imekuwa ikibadilikabadilika.

Habari kutoka kwa chanzo chetu makini ambacho ni ndugu wa karibu na familia hiyo, kwa sharti la kutotajwa gazetini alisema, afya yake bado haijaimarika tangu aliporejea kutoka nchini India alipokuwa akipatiwa matibabu katika Hospitali ya Appolo.


CHANZO KINATIRIRIKA

“Hili suala ni la kifamilia zaidi na linafanyika kwa siri sana, kwahiyo usinitaje mahali popote...kiukweli hali ya Vengu bado hairidhishi. Tangu amefika tumejitahidi sana kumfanyisha mazoezi kama tulivyoelekezwa na madaktari wake lakini wapi!
“Anaumwa na kwa kweli sisi kama wanandugu tumechanganyikiwa sana. Tumekaa vikao na kujadiliana, maana wengi tulikuwa tumependekeza arudishe tena Appolo aendelee na matibabu lakini wengine wamekataa.




“Mvutano ni mkubwa, maana wanaotaka atibiwe hapa wanasema ni kwa sababu alishakwenda huko India na amerudi bila matumaini. Kwa hiyo wote tumeungana nao, kwa sasa tunaangalia namna nyingine ya kumshughulikia matibabu akiwa hapa hapa nchini.”



Katika hatua nyingine, memba wa Kundi la Orijino Komedi aliye Mkurugenzi wa wasanii hao, Isaya Mwakilasa ‘Wakuvywanga,’ alithibitisha kuwa Vengu bado ni mgonjwa.

“Sizungumzi kama Mkurugenzi wa Orijino Komedi lakini ukweli, jamaa bado anaumwa, nadhani juhudi za kumpatia tiba zaidi  zinapaswa kufanyika mara moja,” alisema Wakuvywanga.


KALAMU YA MHARIRI

Kuugua ni sehemu ya maisha ya binadamu. Ni mapito ambayo tunaamini yana mwisho wake. Dua zetu tunazielekeza kwa Mungu ili ampe ahueni ndugu yetu Vengu. Aendelee kuwapa ndugu zake moyo wa upendo na subira wakati huu wa kumuuguza.









No comments:

Post a Comment

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...