Saturday, May 19, 2012

Kanisa la ajabu




WAKATI imezoeleka kwamba makanisa mengi hukusanya waumini kila Jumamosi, Jumapili achilia mbali siku za katikati ya wiki, HOT POT limegundua kanisa ambalo waumini wake wanaishi nje ya nchi na huja kila Desemba 24 kwa ajili ya ibada moja tu.
Kanisa hilo lililopo Mbuyuni, Kata ya Wazo Mtaa wa Salasala, Wilaya ya Kinondoni jijini Dar es Salaam, inadaiwa kuwa waumini wake wanatokea Ugiriki wakiwa ni Wakristo wa madhehebu mbalimbali.
Habari zinasema kuwa kuna Wakatoliki, Walokole na Waanglikana ambao husali pamoja katika kanisa hilo.
“Wakishafanya ibada yao ya Sikukuu ya Krismasi hurudi kwao na kanisa hufungwa mpaka mwaka unaofuata,” kilisema chanzo chetu kimoja.
Mbali ya milango ya kanisa hilo kufungwa baada ya waumini hao kuondoka lakini kuna mtu anayefanya usafi kwa ajili ya kulitunza kanisa hilo.
Pia, askari wa Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) ambao hufanya shughuli zao karibu na sehemu lilipo kanisa hilo, huchangia kuliwekea ulinzi saa nyingine bila kujitambua.
Waandishi wa gazeti hili walipofuatilia, walibaini kuwa linamilikiwa na mwanamke wa Kigiriki aliyefahamika kwa jina moja la Stella (70). Pia, ilifahamika kuwa awali, kanisa hilo lilikuwa likimilikiwa na raia wa Kigiriki aitwaye Mitili ambaye alipofariki dunia aliwaachia urithi wanae wawili ambapo mmoja wao ni Stella.
Jitihada za waandishi wetu kuzungumza na Stella ziligonga mwamba baada ya kuambiwa amesafiri kwenda Ugiriki.
Risasi likapiga kiguu na njia hadi kwa Mwenyekiti wa Serikali ya Mtaa wa Salasala, Kayenge Mshindo ambaye alishangaa na kusema kuwa hajui chochote kuhusiana na kanisa hilo, akaomba apewe muda wa kulifanyia kazi.

VIONGOZI WA MAKANISA WANASEMAJE?
Baadhi ya viongozi wa makanisa, walizungumza kuhusu uwepo wa kanisa hilo linaloonekana kuwa la ajabu.
Wa kwanza alikuwa ni Nabii Flora Peter kiongozi wa Kanisa la Maombezi Mbezi Beach jijini Dar, ambaye alivitaka vyombo vya usalama kulifanyia kazi suala hilo.
Naye, Askofu Mkuu wa Kanisa la Full Gospel  Fellowship, Zachary Kakobe, alisema hana cha kuzungumzia kwani kila kukicha watu wanaanzisha makanisa.
Mchungaji wa kanisa la Assemblies of God, Getrude Rwakatare lilipo Mikocheni B, Dar alisema kuwa kanisa hilo halijui lakini kama lipo serikali ifanyie uchunguzi kwa ajili ya usalama wa taifa.
Kiongozi wa Kanisa la Living Water Center, Mtume Onesmo Ndege: “Hilo siyo kanisa kwani haiwezekani waumini wakawa wanaabudu mara moja kwa mwaka, isipokuwa ni dini ya kundi la watu wachache na wanajua nini wanachokiabudu.”
Kiongozi wa  Kanisa la Christian Mission  Fellowship, Mchungaji Antony Lusekelo ‘Mzee wa Upako’: “Sijui chochote kuhusu kanisa hilo lakini Watanzania wanatakiwa kuwa macho katika kipindi hiki ni cha nyakati za mwisho.”

No comments:

Post a Comment

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...