Wednesday, November 23, 2011

MAISHA: Nguvu tano muhimu kwa mwanadamu kuwa nazo



Wengi wetu tuna ndoto za kuwa watu wenye nguvu katika jamii tunazoishi. Kama ukifanya uchunguzi kwa watu kumi tu waliopo karibu yako utagundua kuwa wanapenda kupata uwezo zaidi ya ule waliona sasa, kitakachowatofautisha ni aina za uwezo wanaouhitaji katika maisha yao. Wapo wenye kutamani kuwa wacheza mpira zaidi ya uwezo walionao, wapiganaji mahiri, matajiri, wasomi na wasanii maarufu.


Kimsingi kila mmoja anahitaji kuwa zaidi ya alivyo sasa, kwa vile mabadiliko hasa ya kimafanikio ndiyo jicho la kila mmoja wetu. Lakini swali gumu linalowashinda wengi kufanikisha tamaa za kuwa na nguvu au uwezo kwenye jamii zao ni jinsi ya kufanya ili wawe kama watakavyo. 



Kama nilivyotaja awali kwamba kuna nguvu za aina nyingi miongoni mwa wanadamu, lakini nguvu tano tunazokwenda kuziangalia ni muhimu kwa mwanadamu kuwa nazo na zinaweza pia kutumika kama njia ya kupata nguvu nyingine zaidi.



Tuanze kwa kuangali nguvu ya kwanza iitwayo The power influencing others au nguvu ya USHAWISHI. 

Katika jamii yetu kuna watu hodari sana kushawishi wenzao, wagome, wafanye uasi waibe, waue na hata wasome kwa bidii. Hata kwenye siasa ili mtu akubalike zaidi anatakiwa kuwa na nguvu hii.



Aina nyingine inaitwa nguvu ya MAPENZI The power of love. Kuna watu hawana pesa kabisa, lakini wana nguvu ya kupendwa, kila wakiingia mahali wanakuwa nyota, wanawavutia wengi. Hivyo ni jukumu la binadamu kuhakikisha kuwa anapata nguvu hii pia na kuitumia katika maisha yake.



Nyingine ni ya UFAHAMU The power of Knowledge, hii inatokana na ufahamu wa mtu juu ya mambo yakiwemo masomo. Katika familia na jamii tunaona kuna watu ambao huaminiwa na wengi na kuwa vinara wa kuulizwa juu ya ufumbuzi wa matatizo au vitu fulani kwa vile wanajua mambo mengi yahusuyo maisha. 



Nguvu nyingine ni ile ya JAMII, Social Power. Bila shaka tumepata kusikia jamii ikisimama na kumtetea mtu kwa maandamano hata kama mwenyewe yuko kifungoni. Nguvu hii inategemea wingi wa marafiki zako kwenye jamii unayoishi. Nyingine ni ya UJUZI ‘Skill power’. Wengi wetu tunakuwa wanyonge kimaisha na kushindwa katika mengi kwa sababu hatuna nguvu hii inayoweza kutupa nafasi ya kukabiliana na maisha, ndiyo maana tumesikia wenzetu wakiamua kujiua pale tu walipokutana na ugumu au kikwazo kidogo cha kimaisha.



Kitaalamu ipo pia nguvu ya MAFANIKIO, The power of Success. Unapokuwa unapata mafanikio zaidi katika maisha yako unakuwa na nguvu ndani ya jamii yako kwa vile wengi watakutazama wewe kama mfano wa mafaniko na hivyo kujipatia wafuasi watakao kuwa nyuma yako. 



Baada ya kutoa mifano hiyo michache ya nguvu ambayo wengi wetu tunapenda kuipata kwenye jamii zetu nitakuwa nimebakiza jibu la swali UNAWEZAJE KUWA MWENYE NGUVU KATIKA JAMII? 



Siri ya kuwa mwenye nguvu katika jamii ni moja tu nayo ni kufanya vitu kwa nguvu, usahihi na umakini mkubwa, ili wengine wakuamini bila kukutilia shaka yoyote. Jibu hili halitofautishi aina ya nguvu tulizozitaja au zile ambazo hatukuzigusia katika somo hili.



Tatizo kubwa miongoni mwa wengi ni kutaka kuwa na nguvu bila kutenda mambo kwa usahihi. Tufahamu kuwa ukitaka kuwa na ushawishi lazima watu wakuamini, ili wakupende unatakiwa kuishi kwa wema, uwe na marafiki lazima uwavutie kwa tabia zako, uwe mwanajamii kwa kujitolea, ujuzi utafute kwa kusoma na kujifunza kila siku, mafaniko yatafute kwa bidii sana bila kuchoka. JAMII IKIKUAMINI KWA MATENDO YAKO, UTAKUWA NA NGUVU. 

No comments:

Post a Comment

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...