Saturday, April 28, 2012

TASWIRA YA KANUMBA NYUMBANI: Mama KANUMBA apata mshtuko...





Katika tukio bichi kabisa, mapema wiki hii, mama Kanumba alipata mshtuko uliomsababishia kupandwa na presha baada ya kuingia chumbani kwa marehemu na kukumbana na taswira ya picha ya marehemu.

Kwa mujibu wa chanzo chetu, mama huyo alishatoa agizo kwa wanafamilia kuzifunika ukutani picha zote za marehemu zilizomo ndani ili asiweze kumwona mwanaye ambaye aliaga dunia ghafla.


Ikasemekana kuwa siku ya tukio la wiki hii, mama Kanumba alifungua mlango wa chumba cha marehemu na kukutana uso kwa uso na picha kubwa iliyokuwa ukutani jambo ambalo lilimshtua sana.

“Alikuwa anaingia chumbani kwa marehemu, ile anafungua tu mlango ukutani akakumbana na picha ya marehemu, akashtuka, presha ikampanda. Maskini, sijui nani aliyeigeuza ile picha wakati mwenyewe alishaamuru picha zote zifunikwe ili asizione,” kilisema chanzo chetu.

Kikaendelea: Tangu alipopata taarifa za kifo cha mwanaye, mama Kanumba amekuwa mtu wa kupandwa na presha, kupoteza fahamu na kutundikiwa dripu, hivyo anatakiwa kuombewa sana.

MLOLONGO WA MATUKIO
Kwa mujibu wa taarifa za ndani, tukio la kwanza la mama huyo kupoteza fahamu ni lili lillilotokea Uwanja wa Ndege wa Mwalimu Julius Nyerere, Dar es Salaam, Aprili 8, mwaka huu alipotua akitokea Bukoba, Kagera ambako ndiko alikopatia taarifa za kifo cha mwanaye. (angalia picha ya ukurasa wa kwanza).


Waombolezaji waliokwenda kumpokea, akiwemo mama wa nyota wa filamu, Vincent Kigosi ‘Ray’, Mary Kigosi walifanya kazi ya ziada kumpatia huduma ya dharura ili arejee katika hali yake ya kawaida.

MAISHA NYUMBANI KWA KANUMBA
Kuna ushahidi wa kutosha kwamba ndani ya nyumba ya marehemu ambapo mama Kanumba yupo kwa sasa, Sinza ya Vatican City Hotel, jijini Dar picha zote za marehemu, hata ile iliyotumika kwenye utambulisho wa jeneza na meza ya viongozi kuandika kitabu cha kumbukumbu, zimefunikwa ukutani.


Ndugu mmoja wa karibu alisema mbele ya mama wa marehemu kuwa mama huyo amekuwa akipata tatizo la presha kupanda mara kwa mara na kutundikiwa dripu ambapo katika moja ya vyumba ndani ya nyumba hiyo kuna chupa za dripu zilizokwishatumika.

ANAISHI KWA USHAURI
Habari zaidi zikasema kuwa, mama huyo ameshauriwa kuishi na maji ya kunywa karibu ili kupambana na tatizo la presha za mara kwa mara.

Watu wa karibu wanasema mara kadhaa mama wa marehemu anakuwa kawaida, lakini linapokuja suala la kumzungumzia mwanaye, hubadilika sura na kuagiza maji au soda ili kujiweka sawa.

“Mara nyingi hataki mambo yanayomhusu marehemu, ikitokea anawahi kusema ongeeni na Seth (akimaanisha mdogo wa marehemu) ili asijiingize kwenye mawazo ya kumuwaza mwanaye.

KINACHOMTESA KWA SASA
Kwa mujibu wa ndugu wa karibu, mama huyo kwa sasa anateswa na uhaba wa watu, inapotokea hakuna watu wanaoingia zaidi ya yeye na familia yenye watu wasiozidi sita, ndipo anapokubali kuwa mwanaye amefariki dunia na kuzikwa,  hivyo hurejesha kilio upya.

STAILI YA KIFO NDIYO INAYOMTESA ZAIDI MAMA 
Jumatano ya wiki hii, paparazi wetu alipata nafasi ya kuongea na mwanafamilia mmoja wa marehemu, nje ya nyumba, ambapo alimuuliza maoni ya mama wa marehemu kuhusiana na kifo cha mwanaye ambapo alisema:

“Mama wa marehemu anakiri kifo kipo, lakini kwa mwanaye anaona afadhali angeugua hata kwa siku moja akili ingekubali kuwa kuna kupona na kufa, lakini ile kuzimika kama mshumaa kunamsumbua zaidi.

WITO KWA VIONGOZI WA DINI 
Kifo kimeumbwa, lakini kusahau pia kumeletwa kwa wanadamu, hivyo baadhi ya watu wamewataka viongozi wa dini kwenda nyumbani kwa marehemu na kumfanyia maombi mama Kanumba ili Mungu afute kumbukumbu za kifo cha mwanaye haraka.

LICHA YA KUUMWA: Sajuki aingia mzigoni...



Licha ya kwamba afya ya msanii wa filamu za Kibongo, Juma Kilowoko ‘Sajuki’ bado hairidhishi kutokana na maradhi yanayomsumbua, juzikati staa huyo na mkewe Wastara Juma walinaswa ‘lokesheni’ wakiendelea kurekodi filamu yao.

Paparazi wetu aliwanasa wanandoa hao wakiwa na baadhi ya wasanii maeneo ya Tegeta jijini Dar ambako walikuwa wakishuti filamu iliyopewa jina la Wakili huku Sajuki akiwa ndiye muongozaji.

Akizungumza, Sajuki alikiri kuwa afya yake bado siyo nzuri lakini ameona badala ya kukaa ndani ni vyema akajishughulisha ili kukabiliana na ugumu wa maisha.

“Bado hali yangu si nzuri lakini kama mtu unaumwa na huna kitu kingine cha kukusaidia katika maisha lazima uwajibike, naumwa lakini siwezi kukaa nyumbani kwa sababu kila dakika moja ya maisha yangu inahitaji fedha,” alisema Sajuki.


Naye Wastara alisema kuwa, afya ya mumewe bado hairidhishi ndiyo maana wameamua kuingia mzigoni ili kuhakikisha wanapata fedha kwa ajili ya matibabu.

 “Kama unavyomuona mume wangu, kimsingi anaumwa na zinahitaji fedha kwa ajili ya matibabu yake na kujikimu pia, ndiyo maana unatuona tumeamua kuendelea na shughuli zetu za kisanii kwani bila kufanya hivi tutakwama katika mambo mengi.


“Hata hivyo, bado tunahitaji msaada ili tuweze kufanikisha matibabu ya Sajuki ambaye tunatarajia kumpeleka India haraka iwezekanavyo,” alisema Wastara.


WADAU TUMSAIDIENI SAJUKI
Kufuatia hali ilivyo, wadau tujitokeze kumchangia Sajuki fedha kwa ajili ya matibabu kupitia simu ya mkononi kwa kutuma kwenye Tigo Pesa namba 0713 666 113 au kwenye akaunti namba 050000003047 katika Benki ya Akiba Commercial yenye jina la Wastara Juma Issa.

KABURI LA KANUMBA LAKARABATIWA



kabuli la kanumba lililoibwa mashada

‘ICON’ katika tasnia ya filamu Bongo, Irene Uwoya na mwenzake Steven Mengere ‘Steve Nyerere’ hivi karibuni walimtafuta fundi na kwenda kulifanyia ukarabati kaburi la staa mwenzao marehemu Steven Kanumba.

Akizungumza na Ijumaa mmoja wa watu wanaojihusisha na kazi ya uchimbaji makaburi eneo la Kinondoni Dar, aliyejitambulisha kwa jina la Kidevu, alisema Ijumaa ya wiki iyopita alishuhudia mafundi wakilikarabati kaburi hilo huku Uwoya na Steve wakiwa pembeni.

“Baada ya lile kaburi kupasuka na kuanza kutitia, juzi niliwaona mafundi wakilikarabati huku pembeni wakiwa wamesimama waigizaji wawili yule mfupi anayeiga sauti ya Nyerere na Uwoya,” alisema Kidevu.
Akizungumzia hilo, Steve Nyerere alisema:
“Ni kweli mimi na Irene tuliamua kulikarabati kaburi la Kanumba baada ya kusoma gazetini kwamba limeanza kutitia.

MAHABA: Uko kwenye uhusiano wa aina gani??





INAWEZEKANA kabisa upo kwenye uhusiano na mpenzi wako kwa muda mrefu sasa, lakini hujui upo katika penzi la aina gani. Si ajabu upo na mtu ambaye kichwani mwake anawaza kukuacha kesho, lakini akilini mwako unapanga kuoana naye!

Lazima uchunguze kwa makini uhusiano wako. Umjue vizuri mwenzi wako, maana matapeli ni wengi siku hizi. Mapenzi ya siku hizi yamejaa ulaghai mtupu, hayana ukweli, kila siku ni maumivu juu ya maumivu.

Matatizo mengi yanaweza kutokea ikiwa utakosa uaminifu kwa mpenzi wako, wakati mwingine matatizo hayo huweza kumlenga mwenzi wako moja kwa moja bila kukusumbua wewe lakini mwisho wa siku wewe utakuja kuwa na matatizo zaidi ya hayo unayoyafanya nyuma ya pazia hivi sasa.

Unaweza kujifanya mjanja sana kwa kuunganisha wapenzi zaidi ya kumi huko gizani ukiamini huonekani na hakuna matatizo yoyote ambayo unaweza kuyapata, kumbe unajidanganya maana  kuna siku utakuja kuumbuka kwa kuonekana kwako huna uaminifu!

Wewe ukoje? Uko kwenye uhusiano wa aina gani? Kuna nuru ya kuingia kwenye ndoa au ni kupotezeana muda tu? Utaendelea kuwa chombo cha starehe hadi lini? Hebu twende darasani tukaone.

USANII UKO HIVI!
Wapo wenye mapenzi ya usoni, moyoni hawana pendo. Wana alama nyingi; wana tabia ya kutamka maneno ya mapenzi lakini ndani ya moyo wake kuna vitu viwili, kwanza anakutamani wewe na fedha zako na wakati huo huo anatamani kuwa na bwana mwingine kwa ajili ya kuongeza kitega uchumi.

Mwanamke wa aina hii siyo ngumu kwake kukuita majina mazuri ya kimapenzi lakini akiwa hamaanishi kutoka moyoni mwake kwamba anakupenda. Hawa wapo wengi lakini ni vigumu sana kuwagundua mapema.

Ngoja nikuulize wewe unayemsaliti mpenzi wako, unavyomfanyia mwenzako hivyo unadhani yeye hana moyo? Hivi hujui kuwa mwenzako anakupenda kwa mapenzi yake yote na amekuchagua wewe uwe mwandani wake?

Siku akijiua kwa sababu yako utakuwa katika hali gani? Hebu acha utapeli wako wa mapenzi haraka sana!

Kuwa muwazi na kama unadhani haupo tayari kuwa na mpenzi basi mwache huru atafute mwingine mwenye msimamo uendelee na mambo yako na kama ni kujiuza ujiuze vizuri lakini ukijua kuwa siku moja utakuja kuingia mahali pabaya. Achana na tamaa za muda mfupi ambazo mwisho wake ni mbaya.

Huyo mwanaume anayekudanganya leo, ujue kabisa kesho hayupo na wewe! Kama umeamua kuwa kiruka njia, mwache mwenzako atafute wake wa maisha. Siyo kumpotezea muda.

KUNA HILI LA USHAWISHI
Hili  ni tatizo lingine linalochochea kuharibu maana ya mapenzi. Ushawishi ni sumu nyingine katika hili. Hapa nitazungumizia pande mbili; mosi ni ya mshawishi na mshawishiwa!

Naweza kusema wote wana makosa maana anayeshawishi hutumia kila njia kumpata anayemhitaji lakini wakati huo huo anayeshawishiwa kukubali wakati akijua ana mpenzi ni kosa kubwa sana.

Wanaume wengi watu wazima tena wenye familia zao hivi sasa ndiyo wanaoongoza kutafuta dogodogo wakidai kuwa damu zao zinachemka! Hutumia fedha, magari na kila aina ya vishawishi ili waweze kuwanasa wasichana hao wadogo wakitafuta penzi. Sijui kama wanaume wa aina hii wanatafuta nini kwa hao mabinti? Hivi kama ukigundua mkeo anakusaliti utajisikije?

Wewe unayewarubuni wasichana ambao wapo masomoni na kuwashawishi kwa fedha zako je, kama ni mwanao ndiyo angekuwa anafanyiwa hivyo ungejisikiaje? Kwa nini unakuwa na moyo wa chuma kiasi hicho?

Ni ulimbukeni wa ajabu sana kumuacha mkeo nyumbani halafu uanze kuhangaika  na vimada. Wa kazi gani kwanza? Labda unatafuta penzi shatashata, sasa si bora umfundishe mkeo akufanyie hayo unayoyapenda? Kwani umemwambia unachotaka akashindwa kukupa?

Unapaswa kubadilika ndugu yangu maana dunia ya sasa siyo ya kuchezea! Kutoka nje ya ndoa siyo suluhisho. Upande wa pili ni wa wasichana ambao hushawishiwa na watu wazima, asilimia kubwa ya wasichana wa aina hii huwa na wapenzi wao, lakini kwa tamaa ya fedha hujikuta wakijitumbikiza katika uhusiano na wanaume hao.

Kwanza hivi wewe binti hujipendi? Kwa nini unaiacha akili yako bila kufanya kazi kiasi hicho? Hebu jiulize, mpaka amekufuata wewe ameshatembea na mabinti wangapi kama wewe? Kitu gani kilichomvutia kwako na wewe umevutiwa na nini wakati una mpenzi wako anayekupenda kwa dhati?

Hebu chekecha kichwa chako vizuri, mpenzi wako ameshakuvisha pete ya uchumba lakini unamsaliti ukijua wazi kuwa unafanya makosa kwa nini unafanya hivyo? Tamaa ya fedha ndogo ndogo itakufikisha wapi?

Acha kuudhulumu moyo wa mpenzi wako, magonjwa siku hizi ni mengi, unatakiwa kutulia na kuachana na tabia zisizofaa ili mwishoni uweze kuwa bora kwa mwandani wako.
Natamani kuendelea na darasa letu, lakini nafasi yangu haitoshi. Naweka kituo kikubwa hapa, wiki ijayo tutaendelea. Si KUKOSA!

JOKATE, DIAMOND SIYO SIRI TENA



Kile kitendawili kwenye Wimbo wa Nimpende Nani wa mwanamuziki Naseeb Abdul Jumaa ‘Diamond Platinumz,’ kimeteguliwa na sasa siyo siri tena kuwa mkali huyo wa Bongo Fleva anatoka kimapenzi na Miss Tanzania namba 2, 2006/07, Jokate Mwegelo (pichani)...

Ama kweli penzi ni kikohozi kulificha huwezi! Habari inayotamba kwa sasa ni kuwa baada ya kujitahidi kuficha uhusiano wao kwa muda mrefu, mwanzoni mwa wiki hii uzalendo ulimshinda Diamond na kujikuta akiweka kweupe kuwa ni kweli Jokate ni wa kwake....

KWENYE MTANDAO WA BBM
Diamond alitumia mtandao wa BBM kuthibitisha kuwa anampenda Jokate kupita maelezo ambapo aliandika ‘No wan can take your place Kate.. I love you so much my baby..’, jambo lililoibua mshtuko kwa waliyoona maneno ya Diamond ambaye bila shaka ndiye msanii namba moja kwa sasa Bongo.

HABARI ZASAMBAA
Baada ya Diamond kuweka maneno hayo, ghafla habari hiyo ilisambaa kama moto wa kifuu kwenye mitandao mingi ndani na nje ya Bongo huku ikipokelewa kwa hisia tofauti.
Kuna waliowapongeza na kuisifia ‘kapo’ yao lakini kuna walihoji kuwa mbona walikuwa wakibisha kuwa hawana uhusiano wa kimapenzi huku Diamond akimuita Jokate dada.
“Watu tuliamini kuwa kitendo cha Jokate kushiriki kwenye video ya Wimbo wa Mawazo wa Diamond ndicho kilichomponza hadi kuhisiwa anatoka na staa huyo, tulidhani anaonewa kumbe ni kweli,” ilisomeka sehemu ya maoni ya mmoja wa watu waliobahatika kuisoma ‘status’ hiyo ya Diamond.

HUYU HAPA DIAMOND
Kutaka kuthibitisha kile alichoandika Diamond kwenye BBM na kusambaa mitandaoni, hot pot lilimvutia waya na kumuuliza ukweli wa habari hiyo ya kumwanika Jokate kuwa ni mpenzi wake ambapo kwa mara ya kwanza alikiri kutoka na mwanadada huyo akisema:
“Ni kweli niko in love (ndani ya penzi) na Kate (Jokate) ila bado sijapanga siku ya kumtambulisha rasmi kwa mashabiki wangu ili wamfahamu shemeji yao.”

MANENO MAZITO
Alipotakiwa kuthibitisha kile alichokisema kwa kutoa ufafanuzi wa ndani, Diamond alikatisha mazungumzo kwa kusisitiza: “Nampenda sana Jokate, hakuna wa kuchukua nafasi yake.”

JOKATE VIPI?
Kupata mzani wa habari hiyo, hot pot  ilimtafuta Jokate ili kusikia neno lake juu ya kuwa ubavu wa Diamond lakini hakupatikana. Akipatikana naye atatoa neno lake.

TUMEFIKAJE HAPA?
Mwaka 2010 wakati Diamond alipozoa tuzo tatu za muziki za Kili, hot pot lilimnasa kwenye picha ya pozi na Jokate ambaye ni mwigizaji, modo na mtangazaji lakini alipoulizwa kama kuna kitu, alisema hakuna chochote kati yao (picha za tukio tunazo).

WEMA VS JOKATE
Mwishoni mwa mwaka jana, aliyekuwa mchumba wa Diamond, Wema Isaac Sepetu alitangaza vita na Jokate akimtuhumu kumwingilia kwenye himaya yake ya kimapenzi.

KUTOKA HOT POT
Timu ya  HOT POT  inaamini kuwa ‘kapo’ ya Diamond na Jokate ni maua yanayopendezesha ulimwengu wa mastaa wa Kibongo hivyo tunawatakia kila la kheri.
Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...